Umoja wa Mataifa waelezea wasiwasi kuhusu raia wa Tigray
Umoja wa mataifa umesema kuwa unaendelea kuwa na wasiwasi kuhusu hali ya raia katika eneo la Tigray nchini Ethiopia.
Kwa mara nyingine umoja huo wa mataifa umetoa wito kwa serikali kuruhusu mashirika mbalimbali kuingia katika eneo hilo ili kuchunguzwa kwa madai ya uhalifu wa kivita.
Kamishna wa umoja wa mataifa anayehusika na maswala ya haki za binadamu Michelle Bachelet, alisema kuwa jumbe mbili za kukagua hali ya kibinadamu katika eneo hilo zilifanikiwa kuingia siku ya Jumatatu.
Hata hivyo Bachelet alisema kuwa kutokana na masharti yaliyowekwa hawakuweza kuchunguza madai mbalimbali ya mauaji ya kiholela na uporaji wa mali.
Umoja wa mataifa umesema kuwa kulikuwa na ripoti za mara kwa mara za mashambulizi dhidi ya makazi na hospitali mwezi uliopita katika mji wa Humera unaopakana na Eritrea.