Matumaini ya bingwa wa Olimpiki Eliud Kipchoge kuwa mwanaume wa kwanza kunyakua mataji matano ya mbio za London marathon yalikatizwa Jumapili alipambaulia nafasi ya nane kwenye makala ya 40 ya shindano hilo.
Kipchoge ambaye pia anashikilia rekodi ya dunia alianza vyema akiongoza kwa kipindi kirefu lakini akaanza kulemewa katika umbali wa kilomita 35 .
Chipukizi Shura Kitata wa Ethiopia alitwaa ubingwa kwa saa 2 dakika 5 na sekunde 41 baada ya kumpiku Mkenya Vincent Kipchumba mita zikisalia mita 50 kufika ukingoni huku Kipchumba akiridhika katika nafasi ya pili kwa saa 2 dakika 5 na sekunde 42 huku mwethiopia mwingine Sisay Lemma akikamilisha wa tatu kwa saa 2 dakika 5 na sekunde 45.
Kipchoge aliambulia nafasi ya 8 kwa saa 2 dakika 6 na sekunde 49 ikiwa mara yake ya kwanza kushindwa tangu aibuke wa pili katika mbio za Berlin Marathon nyuma ya Wilson Kipsang mwaka 2013.
Ni mara ya kwanza kwa Kitata aliye na umri wa miaka 24 kushinda mbio kuu baada ya kumaliza katika nafasi ya pili katika mbio za Berlin na London marathon.