Halmashauri ya ukusanyaji ushuru nchini, imezindua kampeni ya kuimarisha ulipaji ushuru kwa kuzindua mpango wa ulipaji ushuru kwa hiari-VTDP.
Mpango huo unatoa jukwaa kwa mlipa ushuru kufichua ushuru ambao hajalipa na ambao hapo awali haukuwa umefahamishwa kamishna wa ushuru kwa minajili ya kupunguziwa adhabu na riba ya ushuru huo.
Mpango huu unadhamiriwa kuimarisha ulipaji ushuru kupitia uzingativu wa zoezi hilo.
Akiongea jijini Nairobi baada ya uzinduzi wa mpango huo, kamishna wa halmashauri ya KRA wa ulipaji ushuru wa humu nchini, Rispah Simiyu, aliwahimiza walipaji ushuru kutumia vyema fursa ya kuzinduliwa mpango huo.
Alisema mara ufichuzi kamili wa ushuru ambao haujalipwa utafanywa na ushuru usio na riba kulipwa, walipa ushuru kama hao watafurahia kuondolewa riba na adhabu za ushuru ambao ulikuwa haujalipwa.
Alisema serikali kupitia halmashauri ya KRA imeanzisha mikakati kabambe za kuimarisha ukusanyaji ushuru na kukabilaiana na athari za janga la COVID-19.